Katika safari yetu ya kuzikumbuka bendi mbalimbali nchini, kuna kitu kinaonekana wazi kabisa, katika swala la muziki kwa ujumla tumerudi nyuma sana. Zamani kulikuwa na bendi binafsi, bendi za serikali , bendi za chama tawala na karibu kila mji ulikuwa na zaidi ya bendi moja. Watu walikuwa wachache sana kuliko siku hizi lakini walikuwa na na nafasi za uchaguzi wa burudani kuliko siku hizi. Sababu ni nyingi lakini si nia ya makala hizi kuongelea hayo japo baada ya mzunguko wa nchi nzima pengine italazimika kujiuliza tumefikaje huku tuliko?
Kabla ya kuendelea na safari kuna kitu kiko wazi kinajitokeza, wakati wa awamu tatu za mwanzo za uongozi wa nchi hii, wasanii wa kila mahala walithaminika, ndio maana unakuta kila mkoa kulikuweko na makundi ya muziki ambayo hatimae yaliweza kujitokeza na kufahamika nchi nzima. Siku hizi ni kawaida kabisa viongozi wa juu kusindikizwa na wasanii ‘wakubwa ‘ wa kutoka Dar es Salaam, utadhani huko wanakokwenda hakuna wasanii, au wanaenda nchi nyingine kutangaza sanaa ya nchi yao.
Safari yetu leo inatupeleka mikoa ya kusini, mikoa hii haikuwa nyuma kabisa katika mambo ya muziki, kulikuweko na bendi toka enzi ya mkoloni. Wazee maarufu kama Mzee Moses Nnauye alianzia huku katika harakati zake za kuhamasisha watu kudai uhuru kwa kupitia muziki.
Kati ya bendi ambazo nina kumbukumbu nazo, nianze naWhite Jazz Band, bendi hii masikani yake yalikuwa Lindi mjini. Bendi hii kama zilivyokuwa bendi nyingine ilipitisha wanamuziki wengi lakini kati ya wanamuziki waliokuja kung’aa nchini waliopitia bendi hii ni marehemu Mzee Kasim Mapili. Yeye alianza kupiga muziki katika bendi hii mwaka 1958, kuna kila sababu kuamini kuwa ilikuweko kabla ya mwaka huo.
Katika picha iliyopo hapo chini ni kipande cha gazeti ambacho kinaonyesha mwaka 1947 tayari kulikuwa na bendi Lindi. Lindi hoyeee.

Mwaka 1963 tayari kulikuwa na bendi iliyokuwa inaitwa Jamhuri Jazz Band mjini Lindi, bendi hii ilikuwa mali ya TANU Youth League, au Jumuiya ya Vijana wa TANU. Jamhuri Jazz Band hii ya ilikuweko kabla ya Jamhuri Jazz Band ile ya Tanga ambayo ilijipa jina hilo mwaka 1967. Japo Jamuhuri Jazz band ya Tanga ilianza mwaka 1955 ikiitwa Young Nyamwezi Band. Wakati tukiwa bado Lindi, haiwezekani kutoitaja Mitonga Jazz Band. Bendi hii ilifanya makubwa kwa kutoa mfululizo wa vibao pendwa, kikiwemo Mariana na Sitaoa tena Mchinga, ambavyo vikipigwa mpaka leo kwa wale ambao wanavisikia kwa mara ya kwanza huvipenda.
Album ya wimbo Mariana ilirekodiwa na mafundi mitambo wa Radio Tanzania Dar es Salaam kwenye ukumbi wa Polisi pale Lindi, lakini ubora wake unazishinda nyimbo nyingi zilizorekodiwa kwenye studio za kisasa, jambo linaloonyesha umahiri wa wanamuziki wa bendi hiyo, na umahiri wa mafundi mitambo.
Mariana –Mitonga Jazz Band
Tukitoka Lindi tuingie mji wa Masasi, mji huu nao ulikuwa na bendi nyingi na ni mji ambao umewahi kutoa wanamuziki wengi ambao walikuja kuwa maarufu Afrika ya Mashariki nzima. Tuanze na Masasi Jazz Band, bendi hii ilitoa wanamuziki maarufu kama mpiga kinanda Gerald Nangati, wapiga gitaa la rhythm wawili mahiri, Ally Makunguru aliyekuja kupigia bendi za JKT Kimbunga Stereo, Mlimani Park, International Orchestra Safari Sound, Tanzania Stars, MK Groupna hatimae kuhamia Kenya ambako pia alipiga muziki katika bendi kubwa maarufu za huko. Ally Makunguru alinikuta nikiwa kiongozi wa bendi ndogo Iringa iliyokuwa ikiitwa Chikwala chikwala, nakumbuka siku anajitambulisha alinambia alikuwa ametoka Masasi ambako alikuwa akipiga bendi iliyoitwa Kochoko Jazz Band.

Masasi Jazz Band ndiko alikotoka Charles Ray Kasembe ambaye alichukuliwa huko na kupelekwa Morogoro na Juma Kilaza wa Cuban Marimba Band. Hakukaa sana na Cuban Marimba kwani alihamia Morogoro Jazz Band iliyokuwa chini ya Mbaraka Mwinshehe. Safari ya muziki ilimpeleka pia Dodoma International Orchestra na hatimae akahamia Kenya alikokuwa na bendi yake ya Les Volcano.
Bendi nyingine iliyokuweko Masasi ilikuwa Umoja Jazz Band, pia kulikuweko na TANU Youth League Jazz Band katika mji huo, jambo lililokuwa kawaida katika miji mingi, ni wazi kulikuwa na sera za makusudi za TANU kuhakikisha kila wilaya kuna kuwa na bendi ya vijana wa TANU. Bendi hii ya TANU Youth League Jazz Band ndio ilikuwa bendi ya kwanza ya mwanamuziki mwingine aliyekuja kuwa mpiga solo mahiri sana katika bendi za JKT Kimbunga Stereo na DDC Mlimani Park Orchestra na hatimae TZ Brothers Band, Henry Mkanyia.
Masasi ulikuwa mji mdogo sana wakati huo lakini ulikuwa na bendi nyingi kiasi hiki, na hizi nilizotaja hapa, ni zile zilizoko katika kumbukumbu zangu tu.
Nachingwea nako hakukuwa kimya kulikuwa na bendi iliyoitwa Mondomondo Jazz band, bendi iliyokuwa ikileta burudani kwa wakazi wa mji huo.
Mtwara ulikuwa mji mwingine wa maraha kule kusini mwa Tanzania, toka miaka hiyo mpaka leo Mtwara imeendelea kutoa wanamuziki mahiri ambao wamekuwa waking’aa kitaifa na kimataifa. Kati ya bendi zilizowahi kuweko Mtwara tuanze na bendi iliyochukua jina la mji huo Mtwara Jazz Band, pia mapema baada ya Uhuru ilikuweko bendi iliyoitwa Honolulu Jazz Band. Mamlaka ya Bandari katika miaka ya zamani ilikuwa inajihusisha sana katika michezo na utamaduni, na hapo Mtwara ikaanzisha bendi ilioyoitwa Bandari Mtwara Jazz Band. Lakini pia ziliwahi kuweko bendi nyingine zaidi katika mji huu, kulikuwa pia na Mambo Jazz Band na Bantu Jazz Band.
Kwa leo nimalizie kwa kuitaja bendi iliyokuweko mji ambao hautajwi sana linapokuja swala la bendi nao ni Kilwa Masoko. Mji huu nao ulikuwa na bendi yake iliyoitwaLucky Star Jazz Band. Lakini mji wa KIlwa wenyewe umeweza kutoa wanamuziki ambao hakika waliingiza mchango mkubwa katika muziki wa Tanzania. Nani asiemjua mwana Kilwa maarufu Ahmad Kipande, ambaye ndie alikuwa muanzilishi wa Kilwa Jazz band?
